Ni ukweli usiopingika kuwa ajali zimekuwa ni mwiba mchungu kwa familia, jamii na taifa
kwa ujumla unaoacha kilio, walemavu, yatima, wajane na wagane kila kukicha.
Katika kuunga mkono jitihada za kupunguza ajali barabarani wakali katika muziki wa bongo fleva Mr Blue, Amini, Banaba Boy na Dyna Nyange wameshiriki kurekodi wimbo wao utakaotumika kwenye kampeni ya dereva makini inayolenga kuhamasisha uzingatiaji wa usalama barabarani na kwenye vyombo vya usafiri.
Nilifanya interview na wasanii hao muda mfupi baada ya kumaliza kurekodi wimbo wa dereva makini ambapo Mr Blue anasema “..kwa kweli hili janga limekuwa kubwa sasa hivi, ukiangalia idadi ya watu wanaofairiki au kupata matatizo kila mwaka imezidi kuwa kubwa janga hili imezidi, nawashauri madereva kuwa makini wanapoendesha magari”
Amin yeye anasema “familia nyingi zinapotea kutokana na ajali zikiwa pamoja safarini, na ajali nyingi zinasababishwa na madereva, kutokuwa makini wanapokuwa wanaendesha magari yao”
Banaba Boy “Vizazi vingi tunavyotegemea ndio vije kuwa viongozi ndio wanapata ajali, ndo vianvyooangamia kwakuwa havina upeo wa kuepuka mambo kama hayo”
Wimbo huo umerekodiwa na mtayarishaji wa muziki C9 na anasema “Mimi mwenyewe binafsi nimeshapoteza ndugu yangu, nimepoteza nguvu kazi nyingi sana za wasanii ambao nilikuwa nategemea wangekuja kurekodi na kunipatia kipato”
Dyna anasema “Tunandugu zetu, wasanii wenzetu wanapata ajali na ajali nyingi zinatokana na uzembe kabisa, kwa hiyo nimejitoa kufikisha elimu ya dereva makini ili kupunguza ajali hizo”
Kampeni hiyo ya dereva makini imeandaliwa na Transevents Marketing kwa lengo la kutoa hamasa kwa madereva kuwa makini wanapoendesha magari ili kuwawezesha abiria kufika salama waendako.
Mkurugenzi Mtendaji wa Transevents Marketing Peter Nzunda anasema “Ajali za barabarani nyingi zinatokana na sababu za kibinadamu, asilimia karibu 78 zinasabaishwa na dereva, sasa kama tatizo limeonekana ni dereva tunaona kwamba ni dereva huyu huyu anahitaji kuelimishwa na kupewa hamasa ya kupunguza ajali”
Audio ya wimbo wa dereva makini imesharekodiwa na kinachosubiriwa ni video yake, tazama video ya maelezo yao hapa chini
Dotto Kahindi, @dpkahindi